Jumanne, 8 Aprili 2014

ASKARI WA WANYAMA PORI AUAWA KIKATILI _--MOROGORO



Askari wa wanyamapori wa hifadhi ya mbuga ya Jukumu iliyoko katika Wilaya ya Morogoro, ameuawa kikatili na wengine kujeruhia baada ya kuvamiwa na kundi la wafugaji jamii ya Kisukuma.

 Baadhi ya askari waliojeruhiwa, Yahaya Ramadhani na Khalphan Shabani, walisema tukio hilo lilitokea juzi wakati askari hao wakiwa katika doria nyakati za usiku katika mbuga hiyo.

 Kwa upande wake, Shabani alisema kuwa wakati wakiwa katika doria hiyo, ghafla  walivamiwa na kundi la wafugaji wa jamii ya Kisukuma na kuanza kushambuliwa kwa silaha za aina mbalimbali ikiwamo mikuki na marungu na kusababisha kifo cha askari mwenzao.

Alimtaja askari aliyefariki dunia baada ya kuchomwa mkuki kuwa ni Ramadhani Magengere, ambapo askari watatu walijeruhiwa.

Kwa mujibu wa Shabani, hilo ni tukio la tatu kutokea katika mbuga hiyo.

Hata hivyo, askari huyo wa wanyamapori, alilishutumu Jeshi la Polisi mkoani Morogoro kwa kushindwa kutoa ushirikiano kuhusiana na mauaji hayo licha ya kutolewa taarifa.

 Ofisa Maliasili Mkoa wa Morogoro, Joseph Chuwa, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Chuwa alisema hilo ni tukio la sita kwa askari wa wanyamapori kujeruhiwa hadi kusababisha kifo huku Jeshi la Polisi kutokutoa uzito wa matukio hayo licha ya kupewa taarifa.

 Kamanda wa Polisi mkoani Morogoro, Faustine Shilogile, pia alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kwamba uchunguzi unaendelea wa kuwatafuta wahusika.

Hata hivyo, Kamanda Shilogile aliwataka wananchi kutoa ushirikiano ili kupatikana kwa wahusika hao.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni