Jumatano, 12 Agosti 2015

Serikali yamalizana na wapagazi

Moshi.

Mwandishi wetu.

Serikali imefikia maazimio saba yatakayowawezesha waongoza utalii na wapagazi kupata ujira wao stahiki na kwa wakati.

Katibu mteule wa Chama cha Waongoza Utalii (TGA), James Mong’ateko alisema hayo mjini Moshi jana.

Alisema miongoni mwa maazimio hayo ni  wapagazi kulipwa asilimia 50 ya ujira wao kabla ya kuanza kufanya kazi.

 “Hii ni sahihi kabisa wapagazi kabla ya kuanza safari zao ambazo huchukua kati ya siku saba hadi nane wataweza kuacha nyumbani fedha za matumizi,” alisema.

Alitaja maazimio mengine kuwa ni Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro kuzuia kampuni ambazo hazijasajiliwa kutoa huduma kwa watalii.

Alisema utekelezaji wa maazimio hayo utasaidia waongoza watalii na wapagazi kulipwa mishahara yao halali kwa mujibu wa Tangazo la Serikali, GN 228.

“Kulikuwa na kisingizio ya kuwa gharama kubwa za leseni wanazotozwa kampuni ya utalii ndiyo chanzo cha wao kuwalipa ujira ulio nje ya agizo la Serikali, lakini kwa azimio hili gharama hizo hazitakuwa sababu tena ya kunyimwa haki zetu za msingi,” alisema Mong’ateko.

Mwenyekiti wa TGA, Sadock Johnson aliiomba Serikali kupitia mamlaka zake husika kuhakikisha maazimio hayo yanatekelezwa kama ilivyoafikiwa na pande zote.

Wakili wa TGA, Elikunda Kipoko alisema wataunda kikosi kazi kitakachofuatilia kwa karibu utekelezaji wa maazimio hayo saba.

“Haina haja ya kumtafuta mchawi katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili waongoza utalii na wapagazi tena, baada ya maazimio haya kupatikana kikubwa ni kuhakikisha utekelezaji wake unafanyika haraka kwa manufaa ya wahusika,” alisema Kipoko.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni