Arusha.
Na Filbert Rweyemamu ,
Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro
Nyalandu amesema pamoja na changamoto zinazolikabili Taifa ya kupiga vita
ujangili unaohatarisha uwepo wa tembo nchini,bado sekta ya utalii inaongoza kwa kuingiza fedha nyingi za kigeni.
Alisema hayo mwishoni mwa wiki alipokuwa akitoa
tuzo kwa taasisi mbalimbali barani Afrika zilizotambuliwa kwa kufanya utalii
endelevu, hali inayohakikisha utunzaji wa mazingira, utalii wa kiutamaduni na
kupiga vita ujangili.
Nyalandu alisema kuna ongezeko la idadi ya tembo
kwenye mfumo wa ikolojia ya Hifadhi za Taifa ya Serengeti, Manyara na Tarangire
licha ya idadi yao kupungua Ruangwa na Ruaha. Alizitaja nchi za Marekani,
Ujerumani na China kuwa ni mfano wa kuigwa kwakuwa zimeendelea kusaidia sekta
ya utalii nchini kupiga hatua na kuweka mazingira mazuri ambayo matokeo yake
yanaonekana.
Mkurugenzi wa taasisi ya Traveler’s Eye,Yvonne
Baldwin alisema Tuzo wanazotoa zinalenga kuzifanya kampuni za utalii na taasisi
za uhifadhi kuwa na mitazamo tofauti na kuanza kuwa na utalii unaolenga vizazi
vya sasa na vijavyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za
Taifa Tanzania (Tanapa), Allan Kijazi alisema shirika hilo hutenga Sh70 bilioni
kila mwaka kwa ajili ya shughuli za uhifadhi nchini.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni