Alhamisi, 16 Julai 2015

Mlima Kilimanjaro uwe kiunganishi- Sibusiso




AddMkurugenzi mkuu wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (Tanapa), Allan Kijazi (kulia), akimkabidhi bendera ya Tanzania na ile ya Afrika Kusini, mwanzilishi wa taasisi ya Trek4 Mandela, Richard Mabaso wakati wa tukio la Raia wa Afrika Kusini na mataifa mengine kupanda Mlima Kilimanjaro kwa ajili ya kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwa Nelson Mandela. Picha na Daniel Mjema

Daniel Mjema
Moshi.
Mwafrika wa kwanza kupanda Mlima Everest, Sibusiso Vilan ametaka upandaji wa Mlima Kilimanjaro utumike kuwaunganisha Waafrika na mataifa mengine duniani.
Vilan ambaye ni raia wa Afrika Kusini, alipanda mlima Everest ambao ni mrefu duniani mwaka 2003 na kuwa Mwafrika wa kwanza kufika kileleni mwaka 2005.
Mpanda mlima huyo wa kimataifa alitoa kauli hiyo juzi wakati yeye na wenzake walipoanza safari ya siku sita ya kupanda Mlima Kilimanjaro kwa ajili ya kuchangisha fedha za kusaidia afya ya watoto wa kike.
Kwa sehemu kubwa fedha hizo zitasaidia watoto wa kike 272,000 wa Afrika Kusini pia wa Tanzania wanaoishi katika vijiji vinavyozunguka Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro.
Mbali na kupanda mlima huo kupitia taasisi ya Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela ya Trek4 Mandela kuchangisha fedha, pia wanapanda mlima huo kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwake kiongozi huyo aliyefariki dunia mwaka juzi.
Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada wa taulo kwa wanafunzi wa kike wa Shule ya Msingi Mazoezi, Vilan alisema mlima huo ni hazina ya dunia ambayo inaweza kuwaunganisha.
Katika hatua nyingine, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (Tanapa), limewaalika waandaaji wa tamthilia mashuhuri ya Isidingo, kuja kuandaa tamthilia hiyo katika hifadhi za taifa nchini.
Mwaliko huo ulitolewa na Mkurugenzi wa Utalii na Masoko wa Tanapa, Ibrahim Mussa wakati wa tukio la kupanda mlima kwa wapandaji 37 kutoka Afrika Kusini.
Miongoni mwa wapandaji hao ni waigizaji maarufu, akiwamo mwigizaji wa tamthilia inayopendwa Afrika ikiwamo Tanzania ya Isidingo, Rajesh Kumar.
Mussa alimwomba Kumar kuangalia uwezekano wa kurekodi tamthilia hiyo katika moja ya hifadhi za taifa nchini kwani hiyo pia itasaidia kuutangaza mlima Kilimanjaro kimataifa.
Kumar alipoulizwa kuhusu mwaliko huo , alisema ataufikisha kwa waandaaji ambao ni Shirika la Utangazaji la Afrika Kusini (SABC). Mkurugenzi Mkuu wa Tanapa, Allan Kijazi alisema tukio la upandaji linalofanywa na Trek4 Mandela litasaidia kuwaunganisha waafrika kwa vile wapandaji sasa wanatoka mataifa mbalimbali.
Mwanzilishi na Mwasisi wa Trek4 Mandela, Richard Mabaso alisema lengo ni kuchangisha fedha zitazowezesha kuwafikia watoto wa kike 272,000 wa Afrika Kusini na Tanzania.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni