Jumatatu, 10 Agosti 2015

‘Vita dhidi ya ujangili ianzie shule za awali’





Arusha.
 
 Mwandishi wetu.

  Elimu ya uhifadhi na vita dhidi ya ujangili imetakiwa kufundishwa kuanzia shule za awali, msingi, sekondari na vyuoni ili kujenga jamii yenye uelewa na rasilimali za Taifa.

Mratibu wa uhifadhi kutoka Taasisi ya The Nature Conservancy inayojihusisha na masuala ya uhifadhi, Alphonce Mallya alisema hiyo ni njia endelevu ya kukabiliana na ujangili unaotishia kutoweka kwa tembo na faru.
Akizungumza katika mashindano ya uchoraji wa picha ya tembo yenye ujumbe wa kupiga vita ujangili kwa wanafunzi wa shule za msingi jijini Arusha jana, Mallya alisema jamii pia inastahili kunufaika moja kwa moja na uhifadhi kupitia Serikali na taasisi zinazohusika na miradi ya maendeleo ya rasilimali.
“Wananchi wanaoishi maeneo ya karibu na hifadhi wataona ni jukumu lao kukabiliana na majangili wanaotishia kutoweka kwa wanyama wetu iwapo watanufaika na miradi itokanayo na mapato ya uhifadhi,” alisema Mallya.
Watoto Samuel Godfrey, Ashraf Omar na Carlos Cosmas kutoka Shule ya Msingi Meru walioibuka washindi katika mashindano hayo yaliyoshirikisha wanafunzi zaidi ya 600 waliwataka wenzao kuwa mabalozi wa vita dhidi ya ujangili kwa kuwafichua ndugu, jamaa na majirani wanaoshiriki vitendo hivyo.
“Tukinyamaza kuwataja majangili tutakuwa sehemu ya wahalifu huo na hatutaona wala kufaidi urithi huu tuliojaliwa na Mungu,” alisema Carlos aliyekuwa mshindi wa jumla.
Watoto wengine waliofanikiwa kufika fainali ni Mariamu Stephen, Frank Fredson na Mohammed Juma wa Shule ya Msingi Burka, Doris Mollel, Godfrey Stephen na Ashraf Athmani kutoka shule ya Ngarenaro.
Jaji Damarice Kilaka alisema mashindano hayo yatafanyika kila mwaka ili kuwajengea uwezo wanafunzi kuhusu hifadhi na vita dhidi ya ujangili nchini.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni