Jumatano, 22 Julai 2015

Kituo cha kulea tembo yatima kina tija kwa Taifa?

Arusha.
Mussa Juma
 Katika hali ya kawaida, Watanzania wamezoea kusikia au kuona vituo vya kulea watoto yatima, ambavyo vimesambaa karibu nchi nzima.
Vituo hivyo vinalea watoto yatima ambao wazazi wao ama wamefariki dunia na kukosa wasimamizi wa familia au kutelekezwa na wazazi.
Baada ya kukithiri kwa mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi, vilianzishwa pia vituo vya kuwalea watoto wenye albinism.
 Waziri wa Maliasili na Utalii ,Lazaro Nyalandu (katikati),akikata utepe kuzindua kituo cha kulea watoto yatima wa tembo ,baada ya mama zao kuuawa kutokana na ujangili  kwenye hifadhi za taifa na mapori ya akiba nchini. Wakanza kulia ni Balozi wa China nchini ,Lu Youqing na kushoto kwa Nyalandu ni Balozi wa Marekani nchini Mark Childress , kulia kwa Waziri ni Balozi wa Ujerumani nchini Egon Konchake na Katibu Mkuuwa Wizara ya Maliasili na Utalii, DkAdelhem Meru .Picha na Filbert Rweyemamu.
 
Hatua hizo, zilichukuliwa ili kulinda maisha ya watoto,hao ambao walikuwa wakivamiwa na kukatwa viungo hata kuuawa na watu wenye imani za kishirikina.
Hata hivyo, baada ya jitihada za Serikali na wadau wengine, mauaji hayo yamedhibitiwa, hivyo watoto kuanza kurejeshwa kwenye makazi yao.
Kurejeshwa kwenye makazi kwa watoto hao, kunatokana na sababu za kitaalamu kuwa kuwalea wakiwa peke yao ni aina nyingine ya kuwatenga, hivyo kuwafanya kuiogopa zaidi jamii inayowazunguka.
Yatima wa tembo
Hata hivyo, katika hali ianyoweza kustaajabisha, Tanzania sasa imeingia katika historia nyingine kwenye sekta ya utalii kwa kuamua kuanzisha vituo vya kulea watoto yatima wa tembo. Tayari kituo hicho cha kipekee kimeanzishwa ili kulea watoto yatima wa tembo, jijini Arusha, jirani na uwanja mdogo wa ndege.
Kituo hicho kimeanzishwa na Taasisi ya African Wildlife Trust kwa lengo la kunusuru maisha ya watoto wa tembo ambao wazazi wao wanauawa na majangili.
Kituo hicho kina vitanda maalumu vya kulala tembo, eneo la kupumzika na eneo dogo la kutembea.
Mkurugenzi wa kituo hicho, Pratik Patel anasema amekianzisha kwa kushirikiana na wadau wengine ili kuokoa maisha ya tembo nchini.
Anasema tembo watoto, ambao wamekuwa wakipoteza wazazi wao kutokana na kuuawa na majangili, wamekuwa pia wakifa.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu ndiye aliyezindua kituo hicho ambapo alieleza kuwa ni faraja kwa Watanzania kuwa na kituo cha aina hiyo.
Anasema nchi nyingine zenye kituo kama hicho ni Kenya na Afrika Kusini.
Nyalandu anasema Serikali inaunga mkono jitihada zozote za kuokoa maisha ya tembo, hata kama ni mmoja.
Anasema kituo hicho, kitaendeshwa kwa usimamizi wa Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania.
“Kituo hiki kimeanzishwa wakati, natoa matokeo ya sensa ya tembo mwaka 2014, ambayo inaeleza kuwa waliopo nchini kwa sasa ni 43,330,” anasema
Anasema idadi hiyo imeongezeka kidogo, kutokana na ukweli kuwa tembo walikuwa wamepungua katika maeneo ya ndani na nje ya hifadhi.
Waziri Nyalandu anasema, tembo watakaolelewa watatunzwa na wakikuwa watarejeshwa kwenye makazi yao ya asili.
“Tunataka kuokoa japo tembo mmoja, lengo la Serikali kwa kushirikiana na wadau wetu, miaka 15 ijayo waongezeke na kufikia 100,000,” anasema Nyalandu.
Tembo wamepungua
Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI), Dk Simon Mduma anasema katika utafiti waliofanya kati ya Mei na Novemba mwaka jana, imebainika tembo kupungua kwenye baadhi ya maeneo na sehemu nyingine kuongezeka.
Anasema historia inaonyesha kwamba Tanzania iliwahi kuwa na tembo zaidi ya 300,000, lakini sensa ya mwaka 2006, walibaki 132,000, mwaka 2009 walibaki 109,000 na sasa wamebainika wapo 43,330.
Wadau wapinga kituo
Wahifadhi wa Wanyamapori, Chama cha Waongoza Watalii (TTGA) na Kituo cha Utafiti wa Tembo Duniani kilicho nchini (WEC) wanaonyesha shaka kuhusu kituo hicho.
Makamu Mwenyekiti wa TTGA, Khalifa Msangi anasema wanahofu kubwa na kituo hicho kwani kinaweza kuwa ni mpango wa kuanzisha eneo la kutunza wanyama mjini (Zuu).
“Kama lengo ni kuwasaidia watoto wa tembo, kwa nini kituo hicho kisingajengwa porini, kwenye maeneo ya asili ya tembo?” anasema.
Anaongeza: “Sisi ni wadau wakubwa wa utalii , tumelijadili suala hili kwenye vikao vyetu na tumekuwa na wasiwasi mkubwa kwa nini kijengwe mjini na katikati ya Arusha?
Je, tembo wakiwa wakubwa watawezaje kurejea porini na kuishi maisha yao ya kawaida kwani muda wote wamekulia mjini?”
“Sisi ni wahifadhi tulitarajia wanyamapori wasaidiwe porini kwani huko ndipo wamezaliwa, kuwaleta mjini ni kuwatenga... kama vituo vya yatima vinafungwa ili watoto walelewe kwenye jamii zao iweje tembo tuwaanzishie vituo vya kuwalea mijini,” anasema
Mkurugenzi wa WEC, Dk Alfred Kikoti anasema ni hatari kuanzisha vituo vya kulea tembo bila kufanyika utafiti wa kutosha.
Hata hivyo, anasema kwa kuwa Serikali ndiyo iliyozindua kituo hicho, anaamini kimesajiliwa na wamiliki wamefuata sheria .
“Hili si jambo geni duniani, lakini nilidhani juhudi zingefanywa katika kulinda tembo, hasa ukanda wa kusini mwa nchi kwenye ujangili mkubwa,” anasema
Anasema hata kungekuwapo sababu ya kujenga kituo hicho, kilipaswa kujengwa ukanda wa kusini, hasa Mikumi ambako kuna tembo watoto wengi ambao wazazi wao wameuawa .
“Suala hili lingeshirikisha wadau wengi hasa wahifadhi na watafiti lingekuwa na dhamira njema zaidi,” anasema.
Mhifadhi John Macha anasema watalii wanapaswa kwenda kwenye hifadhi za taifa na kuruhusu vituo vya aina hii, wanyama kama tembo wanaweza kuwekwa huko ili waje kuona na kurejea makwao.
“Naweza kusema hii ni kama aina nyingine ya ujangili tu, kwani suala hili linahitaji ushirikishwaji mkubwa wa wadau,” anasema
Macha anasema kwa mujibu wa sheria ya hifadhi za taifa, hairuhusiwi kuchukua kitu chochote ndani ya hifadhi na kukipeleka nje ili kulinda ikolojia ya hifadhi.
“Ndiyo sababu hata kinyesi cha tembo hakitakiwi kuchulikuwa. Ukikuta mnyama kagongwa na gari, huwezi kumchukua kwani maisha ya hifadhini mambo hutegemeana,” alisema.
Hata hivyo, swali linalobaki ni: Je, kituo hicho kitasaidia mapambano dhidi ya ujangili au kuibua migogoro mingine katika sekta ya utalii?
Big Brother winner, Idris Sultan acquires new house...

Read More at thenet.ng/2015/01/photos-big-brother-winner-idris-sultan-acquires-new-house/ Follow us: @theNETng on Twitter | theNETng on Facebook

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni